Ads (728x90)

Tabs

Page

Janja
Janja (kulia)
Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
KUANZIA leo tutakuwa kila siku tunawaletea wasifu wa mchezaji mmoja anayechezaji Tanzania. Leo tunaanza na Amour Janja, mshambuliaji hatari aliyetua JKT Ruvu akitokea JKU ya Zanzibar.

Jina kamili: Amour Omary Janja
Kuzaliwa: Julai 7, 1985
Umri: Miaka 29
Mahali: Unguja, Zanzibar
Nafasi: Mshambuliaji
Klabu alizocheza: Gulioni FC, Mlandege FC (zote za Zanzibar), Oljoro JKT ya Arusha, Mtende Rangers FC, Bandari FC, Miembeni FC, JKU FC (zote Zanzibar) na sasa JKT Ruvu.
Mke wake: Savina Nyasa
Mtoto wake: Mohamed Amour
JANJA NI NANI?
Ni mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Zanzibar aliyefunga bao pekee la mechi kali ya robo-fainali ya Kombe la Mapinduzi mwaka huu lililoing’oa Yanga dhidi ya JKU kwenye Uwanja wa Amaan visiwani Zanzibar Januari 8.
Alifunga mabao matatu katika mechi tano za michuano hiyo mwaka huu sawa na William Wadri (KCCA), Andrey Coutinho (Yanga) na Ibrahim Ajibu (Simba). Mabao hayo alizifunga timu tatu za Mafunzo, Mtibwa Sugar na Yanga huku akiweka rekodi ya kuwa mchezaji pekee aliyeifunga Yanga katika michuano hiyo mwaka huu.
Janja, mzaliwa wa Zanzibar, alianza kucheza soka akiwa na timu ya Gulioni visiwani Zanzibar akifundishwa na kocha Yusuph Chunda (sasa Kocha Mkuu wa Shangani FC ya Zanzibar pia) kabla ya kujiunga na Mlandege 2003/4 na kuitumikia kwa misimu miwili kabla ya kutimkia Miembeni, zote za visiwani hapa.
Janja (29) aliwahi kuitumikia Oljoro JKT ya Arusha ikiwa Ligi Daraja la Kwanza (FDL) na kuipandisha VPL akiibuka mfungaji bora wa timu akiwa na wakali wengine kibao wakiwamo Nassoro Masoud ‘Chollo’, Juma Mohamed na Ally Hamza.
Baada ya kutoka Arusha, akajiunga na Mtende aliyoitumikia kwa misimu miwili kabla ya kujiunga na Bandari, lakini timu hiyo ilivunjwa, akatimkia Miembeni ambako aliibuka mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Zanzibar misimu miwili iliyopita akitupia mabao 15. Msimu uliopita alijiunga na JKU na alikuwa mwiba mkali.
Mume huyo wa Savina Nyasa na baba wa mtoto mmoja, Mohamed Amour, ana uwezo mkubwa katika kupiga mashuti ya nje ya boksi.
Ni mtoto huyo wa tatu kuzaliwa katika familia ya watoto sita (watatu wa kiume) ya Bw. Omary Janja na Bi. Rose Musele.
Mguu wake wa kushoto ndiyo hatari zaidi kwa makipa. Janja ana nguvu, mwili ulioshiba, ana kasi na ni mwepesi wa kuchukua uamuzi wa kupiga mashuti ya kushtukiza.
Huyu ndiye Amour Omary Janja, mshambuliaji hatari aliyeing’oa Yanga Kombe la Mapinduzi 2015.

Post a Comment