Ads (728x90)

Tabs

Page

Sehemu ya askari kikosi maalum ikiuvamia Mtaa wa Saint Denis .
sehemu ya askari kikosi maalum ikiuvamia Mtaa wa Saint Denis .
MWANAMKE mmoja amejilipua huku mshukiwa akiuwawa kwa kupigwa risasi wakati wa operesheni ya polisi katika mtaa mmoja wa Saint Denis jijini Paris. Tayari watu saba wamekamatwa kuhusiana na tukio la mashambulizi. Polisi walishambulia nyumba moja mtaa wa Saint Denis wakieleza kuwa mshukiwa anayedaiwa kupanga mashambulio ya kigaidi ya Ijumaa ambayo yalisababisha vifo vya watu 129 mjini Paris. Hatima ya mshukiwa huyo, Abdelhamid Abaaoud, ambaye awali alidhaniwa kuwa nchini Syria bado haijulikani. Mkuu wa mashtaka Francois Molins alisema habari za kijasusi zilikuwa zimedokeza kwamba yumo mjini Paris. Wote waliofariki kwenye mashambulio hayo ya Ijumaa wametambuliwa, serikali imesema.
Kundi la Islamic State (IS) lilisema lilihusika kwenye mashambulio hayo. Operesheni hiyo mtaani Saint – Denis, ambako uwanja wa taifa wa Stade de France unapatikana, ilianza mwendo wa saa kumi na dakika ishirini saa za Ufaransa. Akiongea na wanahabari eneo la operesheni baadaye, Bw. Molins alisema operesheni hiyo ilianzishwa baada ya udukuzi wa simu na habari za kijasusi kudokeza kuwa Abaaoud, Mbelgiji mwenye asili ya Morocco, huenda alikuwa nyumbani humo.
Mwanamashtaka huyo alisema mwanamke mmoja, ambaye kituo cha runinga cha BFMTV cha Ufaransa kilisema alikuwa jamaa wa Abaaoud, alijipua baada ya operesheni kuanza. Mshukiwa mwingine aliuawa na guruneti na risasi za polisi, Bw Molins alisema.

Vikosi vikiwa kazini kuwasaka washukiwa.
Vikosi vikiwa kazini kuwasaka washukiwa.

Maofisa watano wa polisi kikosi maalum cha kupambana na ugaidi cha RAID waliohusika kwenye operesheni hiyo walipata majeraha. Mbwa wa kikosi hicho cha polisi kwa jina Diesel mwenye umri wa miaka saba pia aliuawa. Wanaume watatu walikamatwa katika nyumba hiyo. Wengine wawili walipatikana wakiwa wamejificha kwenye vifusi na wengine wawili, akiwemo mwanamume mmoja aliyekuwa amekodisha nyumba hiyo walikamatwa. Hata hivyo polisi hawakutoa majina ya waliokamatwa. Watu 400 walijeruhiwa kwenye mashambulio yaliotokea Ijumaa, huku watu 221 kati yao bado wanatibiwa hospitalini, 57 kati yao wakiwa wamelazwa kwenye vyumba vya wagonjwa mahututi. Mataifa ya Ulaya yameendelea kuwa katika hali ya tahadhari.
Jumanne, mechi ya kirafiki kati ya Ujerumani na Uholanzi ilifutiliwa mbali muda mfupi kabla ya kuanza na ndege mbili za shirika la Air France zilizokuwa zikielekea Paris kutoka Marekani zilibadilisha njia kutokana na hatari za kiusalama. IS walisema walitekeleza mashambulio hayo kulalamikia operesheni ya ndege za kijeshi za Ufaransa dhidi ya ngome zake Syria, na kuahidi kushambulia zaidi. Rais wa Ufaransa Francois Hollande alisema Jumatano kwamba IS wanatishia ulimwengu wote na kwamba atatafuta “muungano mkubwa” wa kufanya kazi pamoja kuangamiza kabisa wapiganaji hao.

Post a Comment